Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatullah Alireza A’rafi, Mkurugenzi wa Hawza nchini Iran, katika hafla ya uzinduzi wa bidhaa mahiri na zenye msingi wa elimu za Kiislamu, Ustaarabu na Irfani, iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jamiat Aalul-Bayt (amani iwe juu yao) mjini Qum, huku akirejelea mwenendo wa mabadiliko ya hivi karibuni katika sayansi za utambuzi na teknolojia mpya, alisema: Wazo ambalo leo sehemu ya matokeo yake yanazinduliwa ni sehemu ya wazo kubwa zaidi lililoanza takriban miaka 12 hadi 13 iliyopita. Mradi huu uliundwa kwa lengo la kuweka msingi wa harakati ya kielimu katika mipaka ya maarifa na kwa mtazamo wa kimataifa, hususan katika elimu za Kiislamu.
Mkurugenzi wa Hawza za kielimu aliendelea kusema: Harakati hii mwanzoni ilianza ndani ya Jamiat al-Mustafa na katika vituo mbalimbali vya kielimu vya Hawza na vyuo vikuu, lakini katika miaka hii hatukuweza kusonga mbele kama ilivyotarajiwa. Hata hivyo, tumekuwa tukisonga hatua kwa hatua kuelekea lengo hilo, na sasa tunashuhudia ushirikiano kutoka taasisi na mashirika mengine.
Mabadiliko ya sayansi za utambuzi
Mjumbe wa wanazuoni wa Baraza la Walinzi aliendelea kuashiria mabadiliko yajayo katika sayansi za utambuzi na kusema: Sehemu ya mabadiliko haya tayari imejitokeza, na mabadiliko makubwa yako mbele yetu ambayo bila shaka yatakuwa na athari muhimu katika masuala mbalimbali ya kielimu, vyuo vikuu na Hawza. Mabadiliko haya, iwe kama fursa kubwa au kama tishio, yana uwezo mkubwa.
Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza za Kielimu aliongeza kuwa: Kwa upande mmoja, mabadiliko haya yanaweza kuleta mawimbi ya mageuzi makubwa katika eneo la elimu na maarifa ya Kiislamu, jambo ambalo ni fursa kubwa kwa jamii ya Kiislamu. Lakini kama michakato hii haitaongozwa ipasavyo, inaweza pia kuleta vitisho vikubwa katika mfumo wa kielimu na kidini.
Athari ya elimu ya Kiislamu katika mabadiliko ya teknolojia mpya
Ayatullah A’rafi alirejelea athari za pande mbili kati ya elimu za Kiislamu na teknolojia mpya, kwa kusema: Kwa upande mwingine, inatarajiwa kwamba elimu za Kiislamu, mantiki na mjadala wa Kiislamu viwe na athari katika mabadiliko ya sayansi za utambuzi na teknolojia mahiri. Jambo hili pia linapaswa kuzingatiwa katika mipango yetu ya kielimu na utafiti.
Mkurugenzi wa Hawza za kielimu alisisitiza: Mabadiliko na mipango hii yote iko ndani ya mtazamo uliotokana na harakati zinazofanana ndani ya Jamiat al-Mustafa. Lengo letu ni kushiriki katika sayansi za utambuzi na teknolojia mahiri duniani, lakini shughuli hizi lazima ziambatane na mjadala wa Kiislamu, fikra za Ahlul-Bayt (amani iwe juu yao) na mantiki ya Mapinduzi ya Kiislamu. Kwa sasa, shughuli nyingi za kimataifa katika uwanja huu zinaanza, na tunatarajia kuona maendeleo makubwa katika siku zijazo.
Nafasi ya teknolojia mahiri katika kuendeleza na kueneza maarifa ya Kiislamu
Ayatullah A’rafi, akirejelea nafasi ya juu ya Qum katika elimu za Kiislamu na jukumu la teknolojia mahiri katika kuendeleza na kueneza maarifa ya Kiislamu, alisema: Kituo cha utafiti cha Noor, kilichoanzishwa kwa amri na mwongozo wa Kiongozi Mkuu, kimepata mafanikio makubwa katika nyanja mbalimbali za kielimu na utafiti. Kituo hiki bado kiko mstari wa mbele katika harakati za kielimu na kinaendelea kupanua shughuli zake kwenye sekta mbalimbali.
Ayatullah A’rafi alisisitiza umuhimu wa tafiti katika sayansi za utambuzi na teknolojia mahiri, akiongeza: Moja ya malengo makuu ya harakati hii ya kielimu ni kutumia teknolojia mpya kuendeleza tafiti za Kiislamu na kujenga uwezo wa wataalamu pamoja na kulea rasilimali watu katika nyanja hizi kwa mtazamo wa Kiislamu na unaotegemea mjadala wa dini. Hii ni mara ya kwanza ninatoa wazo hili kwa uwazi kwamba katika miaka 20 iliyopita, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji katika uwanja huu, sasa tunalenga kuanzisha kiini cha kwanza cha harakati hii ya kielimu hadi mwaka ujao.
Pia alirejelea hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika mwelekeo huu na kuongeza: Kwa msaada na dua za wote, tunatumaini kwamba harakati hii ya kielimu itakamilika katika miaka ijayo na kusaidia maendeleo ya elimu na ustaarabu wa Kiislamu.
Mihimili muhimu ya akili mnemba kwenye elimu za Kiislamu
Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Ayatullah A’rafi alilinganisha mitazamo miwili kuhusu kuingia kwa teknolojia mahiri katika elimu za Kiislamu na kusema: Teknolojia mahiri lazima ziingie katika uwanja wa elimu na maarifa ya Kiislamu ili, sambamba na kunufaika na nyenzo hizi mpya na fursa zilizopo zitambuliwe na kusimamiwa. Katika muktadha huu, kuna mihimili kadhaa muhimu inayopaswa kuzingatiwa na wanazuoni wa Hawza na vyuo vikuu.
Mkurugenzi wa Hawza za kielimu kisha alieleza mihimili sita muhimu ya kuingia kwa teknolojia mahiri katika elimu za Kiislamu:
Kwanza: Teknolojia mahiri na vyanzo pamoja na matini za msingi za Kiislamu — mojawapo ya maeneo muhimu kwa kuingia akili mnemba katika elimu za Kiislamu ni uchambuzi wa matini za msingi kama Qur’ani Tukufu na Sunna ya Mtume (saww), jambo linalofungua upeo mpya wa elimu ya Kiislamu.
Pili: Teknolojia mahiri na vyanzo pamoja na matini za pili — kwa msingi wa vyanzo vya awali, maelfu ya vitabu na marejeo ya falsafa, teolojia, hadithi, tafsiri na fiqhi yameandikwa, ambayo inahitaji kuchambuliwa kwa kutumia teknolojia mahiri.
Tatu: Teknolojia mahiri na elimu za Kiislamu — teknolojia mahiri zinaweza kuwa na nafasi muhimu katika kuendeleza falsafa, teolojia, tafsiri na fiqhi ya Kiislamu na kufanya tafiti kuwa za kisasa zaidi na zenye ufanisi.
Nne: Teknolojia mahiri na utekelezaji wa fikra za Kiislamu katika maisha ya mwanadamu — mojawapo ya changamoto kubwa ni kuoanisha fikra za Kiislamu na maisha binafsi na ya kijamii ya mwanadamu. Teknolojia mahiri zinaweza kutoa mifano mipya ya kutekeleza misingi ya Kiislamu.
Tano: Teknolojia mahiri na usambazaji wa utafiti wa Kiislamu nchini Iran na duniani — matumizi ya teknolojia hizi katika tablighi na kueneza maarifa ya Kiislamu vinaweza kusaidia kujenga mjadala wa kimataifa na kubadilishana tamaduni.
Sita: Teknolojia mahiri na historia pamoja na ustaarabu wa Kiislamu — akili mnemba inaweza kuwa na nafasi muhimu katika kuhifadhi na kutambulisha historia na ustaarabu wa Kiislamu na kuuwasilisha kwa vizazi vipya.
Ayatullah A’rafi alisema: Mihimili hii inahitaji juhudi endelevu na ushirikiano wa pamoja wa watafiti katika nyanja mbalimbali. Tunapaswa, kwa kutumia teknolojia mahiri, kuinua elimu za Kiislamu hadi kiwango kipya na kumsaidia mwanadamu wa leo kuelewa vizuri zaidi maarifa ya Kiislamu.
Maoni yako